My Blog List

Monday, February 7, 2011




Vijana ndio nguvu kazi inayotegemewa katika kuinua uchumi wa taifa lolote lile. je katiba mpya itawaangalia na hawa pia?

Tuesday, January 11, 2011

HUYU NDIYE MWANDISHI BORA WA FILAMU.

Filamu ni njia mojawapo ya kuburudisha na kuielimisha jamii. Utengenezaji wa filamu katika dunia ya leo unawategemea watu wengi sana, lakini jambo la ajabu na ambalo limekuwa likinitatiza siku nyingi ni kwamba, je ni watu wapi hasa muhimu au ili filamu iweze kukamilika inawahitaji watu wangapi? Bila shaka Mtu wa kwanza kukumbukwa ni Mtayarishaji “Producer”, Mwongozaji “Director”, waigizaji “Actors and actresses”.

Ni nadra sana hasa hapa kwetu watu kumkumbuka mwandishi wa mswada“Script writer” hata waandaaji wa tuzo wamekuwa hawawakumbuki kabisa waandishi watu hawa, utasikia tuzo ya Msanii bora wa kike/ Msanii bora wa kiume, Mwongozaji bora, na wala husikii ikizungumziwa tuzo ya Mwandishi bora wa filamu. Je huo ubora wa waigizaji ama ubora wa waongozaji unatoka wapi au na kazi iliyoandikwa na nani?

Ni ukweli usiopingika kwamba Waigizaji, Waongozaji, na hata Watayarishaji wengi wamepata mafanikio makubwa kwasababu walipata mswada mzuri wa kuufuata
Kwa mtazamo wangu nafikiri mwandishi ni mtu muhimu sana hasa linapokuja suala la utengenezaji wa filamu, hata kufanikiwa kwa mwongozaji ama filamu kunamtegemea mwandishi kwa asilimia kubwa, ukweli ni kwamba hata kama mwongozaji atakuwa bora kiasi gani lakini mswada anaoufuata haukuandikwa, wala kupangiliwa vizuri ni dhahiri kunauwezekano mkubwa wa filamu hiyo kuwa mbaya.

Mahitaji ya filamu hapa Tanzania yamekuwa ni makubwa sana hivyo kufanya soko la filamu kukua kila siku, Ukuaji huo umefanya hata mahitaji ya miswada ya filamu kuongezeka pia. Kutokana na mahitaji kuwa makubwa imejitokeza kasumba ya kila mtu kujiita yeye ni mwandishi wa filamu. Je hao wanaojiita waandishi wa script ni Weledi, Wabunifu ama ni wababaishaji tu na wanaandika ili wapate vijisenti vya kuwawezesha waishi mjini?

Waungwana uandishi wa miswada ya filamu ni kazi ngumu sio kama watu wengi wanavyofikiria, ni kazi inayohitaji muda wa kutosha, hivyo ili mtu aweze kuandika mswada bora na utakaouzika hana budi akazingatia sifa za mwandishi bora wa mswada “ a Professional Script Writer”

KIPAJI “Talent ” ni Kitu cha kwanza anachotakiwa mwandishi wa filamu kuwa nacho, lakini ikumbukwe kuwa kipaji pekee hakitoshi kumfanya mtu kuwa mwandishi bora bali kipaji kikubwa na ubunifu, upeo wa kufikiria mambo vitamwezesha kufika mbali, uandishi wa miswada wa filamu unabadilika kila siku kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia na mahitaji tofauti tofauti wa watazamaji wa filamu, kwahiyo ni vizuri mwandishi akajizoesha kwenda sambamba na mabadiliko yanayotokea kila siku, mbinu mojawapo ni kuwa na moyo wa kujifunza ama kusoma au kuhudhuria semina na mafunzo mbalimbali yanayotolewa na wadau au wasomi mbalimbali, pia hata kuhudhuria kwenye matamasha ya filamu, hii itamwezesha kukutana na kubadilishana uzoefu na waandishi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi.

Uandishi wa filamu sio kwamba unahitaji watu wa aina fulani ama ni kazi ya kundi fulani la watu, la hasha, mtu yoyote anaweza kujifunza na kujiendeleza na kuwa mwandishi bora, kuna shule na vyuo mbali mbali ambavyo vinatoa taaluma ya uandishi wa filamu, hivyo kupitia njia hii mtu anaweza akajiongezea maarifa na ujuzi.
Mwandishi wa filamu ni lazima ajue mahitaji ya jamii anayoiandikia, hili limekuwa tatizo kubwa na sugu kwa waandishi wengi wa miswada ya filamu duniani, wengi wao wamekuwa wanaandika hadithi ambazo haziendani na mazingira halisi ama mahitaji au utamaduni za jamii husika.

Kwa mfano asilimia 75 ya waandishi wa filamu hapa nchini wamekuwa waandika stori ambazo si mahitaji ya jamii ya Tanzania wala hazina maadili wala utamaduni wa kitanzania, wengi wao wanandika hadithi ambazo zinaelezea zaidi maisha ya watu wa ulaya au Afrika ya magaribi.

Ikumbukwe kuwa mwandishi wa filamu ni “ZAO LA JAMII” husika hivyo tunategemea zaidi uandishi wake uzingatie zaidi katika hadithi za maisha ya jamii anayotoka kwa sababu yeye ni mmoja wapo wa wanajamii, hivyo atakuwa anaijua vyema jamii yake bila shaka hata mahitaji ya jamii yake atakuwa anayajua.

Ukiachilia mbali Mwandishi kuwa zao la jamii, mwandishi bora wa filamu ni yule anayejua je ni kundi lipi la jamii amelilenga kuwafikishia ujumbe, ni ukweli usiopingika kuwa kupitia filamu watazamaji wanapata Elimu na burudani pia.
Kwahiyo ujumbe uiopo kwenye filamu ni lazima uende sambamba na mahitaji ya kundi husika.
Mwandishi bora wa filamu anatakiwa kuwa na mawazo mapya, pia akumbuke kuwa uandishi wa miswada ya filamu ni kazi ambayo inawapatia kipato kikubwa waandishi wengi hivyo daima awe ni mtu wa kufikiria kufanya makubwa katika kila kazi anayoiandika, daima alenge kuja na mawazo na mtindo mpya katika kila kazi anayoiandika hii itafanya kazi anazoziandika ziwe na mvuto wa kipekee na hivyo kudumu kwenye jamii kwa muda mrefu.
Daima aweze kusafiri mbali kimawazo zaidi ya vile watazamaji watakavyofikiria, ni dhambi kubwa katika uandishi wa filamu kumpa nafasi mtazamaji wako kuingia ndani ya mawazo katika kazi unayoiandika, andika ukijua kwamba wewe ndio unayemfanya akae na kutizama filamu kuanzia mwanzo mpaka mwisho.

Umakini katika kuchagua vema mtindo wa namna ya kuwasilisha ujumbe ni sifa moja wapo ambayo mwandishi bora wa filamu anatakiwa kuizingatia. Waandishi wengi wanapenda kutumia mtindo wa urejeshi “ flashback’ au mtindo wa moja kwa moja “fore shadowing”, jambo la kuzingatia ni kuwa kila mtindo unafaida na hasara zake, hivyo inampasa mwandishi awe makini sana katika kuchagua ili awasilishe vema ujumbe alioukusudia kwa jamii.

Ukitaka kuwa mwandishi mzuri wa filamu huna budi kuandika mswada utakaowavutia watazamaji na wadau wa tasnia ya filamu, filamu yako ni lazima iweze kuwaburudisha na kuwaelimisha watazamaji kwa huo huo na hasa hasa kuzingatia vile vitu muhimu vinavyotakiwa katika filamu nzuri.

Filamu nzuri ni ile ambayo mwandishi wake ameweza kuyapangilia vizuri matukio na vitendo vingi katika filamu vimeelezea vizuri dhamira ya hadithi nzima, hivyo mwandishi wa filamu anashauriwa aandike vitendo vingi kuliko mazungumzo. Kwani utamu wa filamu ni vitendo na si mazungumzo marefu.

Mwandishi mzuri wa miswada ya filamu ni yule anayeweza kuwashika watazamaji wake kifikra mapema iwezekanavyo, andika mswada ambao utacheza muda wote na fikra za watazamaji wako, daima andika matukio ambayo yatamtamanisha au kumpa hamu mtazamaji na kumfanya asinyanyuke kwenye kiti ama kuzima runinga yake: kwa mfano wahusika wakuu katika filamu yako ni lazima awe anawafurahisha watazamaji wako, kiasi kwamba uwepo wa maadui “Villains” uwafanye pia watazamaji hao hao wanyanyuke kwenye viti hasa pale kunapotokea tukio la kuwakutanisha na kupambana ama kufanya tukio lolote.
Hata Kama unaandika mchezo wa kuigiza, vichekesho, filamu za kutisha, za kisayansi ama za mapenzi kumbuka kwamba siri ya mafanikio ni kuweza kukamata na kusafiri pamoja na fikra za watazamaji wako muda wote.

Uandishi wa miswada ya filamu ni kazi inayotaka mwandishi ajitume sana, awe ni yule mwenye ubunifu wa hali ya juu, upeo mkubwa wa kupambanua mambo, mwenye mawazo mapya katika kila kazi anayoiandika, na anayejua kucheza na saikolojia ya watazamaji wake, kwani uandishi wa filamu unahusisha uwasilishaji wa mtazamo, hisia, matatizo ya jamii inayoandikiwa.

Friday, December 31, 2010

Tuesday, December 28, 2010

6 Reason why people commit suicide.


Though I’ve never lost a friend or family member to suicide, I have lost a patient.
I have known a number of people left behind by the suicide of people close to them, however. Given how much losing my patient affected me, I’ve only been able to guess at the devastation these people have experienced. Pain mixed with guilt, anger, and regret makes for a bitter drink, the taste of which I’ve seen take many months or even years to wash out of some mouths.
The one question everyone has asked without exception, that they ache to have answered more than any other, is simply, why?
Click here to read more;

Tuesday, December 14, 2010

HIVI KWELI ELIMU NI UFUNGUO WA MAISHA?

Ni hali halisi ya shule ya msingi moja iliyoko huko mkoani Morogoro. Wanafunzi wanakaa chini, madarasa yamechoka mpaka basi, chini vumbi tupu yaani hali ni mbaya. Je kuna uwezekano wa shule kama hiyo kutoa wasomi watakao ongoza Taifa hili? tunadanganyana hapa hatoki msomi yoyote?

Wednesday, December 8, 2010

MWONGOZAJI BORA WA FILAMU ANATAKIWA KUWA NA SIFA GANI?

KATIKA Makala yangu ya wiki mbili zilizopita nilizungumzia ni kwa namna gani mtu anaweza kuwa mwongozaji bora wa filamu, ambapo niliziainisha hatua nne za msingi ambazo wale wote walio na ndoto za kuwa waongozaji bora wa filamu hawana budi kuzifuata ili waweze kufanikiwa.

Ikumbukwe kuwa mwongozaji “ Director” anabeba Majukumu, Mamlaka na anayefanya Maamuzi yote yanayohusu ubunifu katika utengenezaji wa filamu, filamu inapokuwa nzuri na kufanikiwa ni mwongozaji anayepongezwa, na ikitokea filamu haikufanikiwa lawama zote zinamwangukia Mwongozaji.

Kwa kuzingatia uzito na majukumu aliyonayo mwongozaji, ni dhahiri nafasi hii inahitaji mtu mwenye ubunifu na weledi wa hali ya juu,

Je mwongozaji wa filamu anatakiwa kuwa na sifa gani?

Mwongozaji wa filamu anatakiwa awe ni msanii wa kweli, anayejua anachokifanya na anachokitaka , ili mwongozaji aweze kufanya jambo zuri ama kazi nzuri anahitaji kuwa na kipaji, ubunifu, moyo wa kujituma na afanye kazi kwa bidii, huku akitambua kuwa kufanikiwa kwa filamu kunamtegemea yenye kwa kiasi kikubwa, na kwamba kipaji pekee hakitoshi kumfanya mtu aweze kuwa mwongozaji bora.

Ni ukweli usiopingika kwamba huwezi kupima wala kujifunza kipaji, bidii katika kazi, mafunzo, mwelekeo na upeo wa kujua nini unataka kufanikisha ni baadhi ya mambo ya msingi ambayo mwongozaji wa filamu anapaswa kuwa nayo na kuyazingatia.

Sifa kubwa ya mwongozaji wa filamu ni “yule anayeongoza kwa mfano” kila mtu anayehusika katika utengenezaji wa filamu mara zote huwa ana mwangalia mwongozaji , huwa anafanya hivyo kwa lengo la kwenda sambamba na kile anacho kihitaji mwongozaji, kwa sababu mwongozaji ndiye anayebeba roho ya filamu. “Carries a Soul of a Film” Mwongozaji anatakiwa kuwa kiongozi na wakati huo huo afikirie ni kwa namna katika abuni na aingize mawazo mapya kadri inavyowezekana katika filamu anayoiongoza ili iweze kuwa na mvuto. daima afikirie ni kwa jinsi gani utafanikisha utengenezaji wa filamu unayoiongoza na namna utakavyo wasiliana na waigizaji na wafanya kazi anaofanya nao kazi.

Mwongozaji anatakiwa kutambua vipaji , uwezo na madhaifu ya kila mtu anayefanya naye kazi ili aweze kujua ni kwa namna gani atayashughulikia na ni kwa ni kwa namna gani atasafiri nao kimawazo hasa hasa katika kuhakikisha mswada wa filamu unawasilishwa kama ulivyokusudiwa,

Mwongozaji anatakiwa kuwa ni yule mwenye “uwezo wa kufanya maamuzi “ yote yanayohusu utengenezaji wa filamu, kufanikiwa kwa filamu kunamtegemea mwongozaji kwa asilimia 100, ingawa maamuzi yanaweza kuwa mazuri kwa upande mmoja na wakati mwingine yasiwe mazuri, yampasa mwongozaji afanye maamuzi hasa pale anapotakiwa na kuna ulazima wa kufanya hivyo, ila maamuzi yanayofanyika yasiwe ya kumkomoa ama kumuumiza mtu yeyote anayefanya naye kazi bali lengo liwe ni kuboresha na kuongezea radha kwa kile kinachotengenezwa.

Mwongozaji anatakiwa awe mbunifu sana, anatakiwa kujua kila kitu kinachotakiwa katika utengenezaji wa filamu hii ikiwa ni pamoja na kuweza kuwaongoza watu wengi, kujua ni kwa namna gani uigizaji , upigaji wa picha, uhariri, mwanga, mavazi, rangi, maneno , muziki, maeneo n.k vitapangiliwa katika filamu anayoiongoza. Kwa ujumla wake mwongozaji ni lazima ajue kila kitu kinachohusu utengenezaji wa filamu

Mwongozaji anatakiwa kuwa na uwezo mkubwa wa kuwasiliana na wale wote anofanya nao kazi, huku akiwashirikisha kila kitu anachowaza na anachokifikiria lengo likiwa ni kuwafanya wote wasafiri katika mawazo yake ili waweze kutengeneza filamu nzuri.

Waongozaji wengi wanapenda kuwa viongozi “ Leaders” na wanajikuta wanasahau kufanya wanachopaswa, Mwongozaji ni kiongozi wa watu wote anaofanya nao kazi katika utengenezaji wa filamu, utengenezaji wa filamu unahitaji umoja na mshikamano miongoni mwa wafanyakazi na waigizaji, mwongozaji anapaswa kuheshimu mawazo na mchango wa kila mtu, hakuna mtu anayeweza kufanya kazi peke yake “a one man show” hasa katika tasnia ya filamu, ushirikiano ni jambo la muhimu kuzingatiwa .

Kufanya kazi pamoja kuna maana kwamba kuna muunganiko wa mawazo ya watu wengi daima penye wengi hapaharibiki jambo na mawazo ya kila mmoja ni muhimu kuzingatiwa na mchango wa kila mmoja ni muhimu sana katika kutengeneza filamu nzuri.

Ni ukweli usiopingika kwamba hakuna muda wa kutosha kufanya kila kitu unachokitaka na unachokifikiria, Waongozaji wengi wamekuwa wakikata tamaa mapema sana hasa pale kazi inapoonekana kuwa ngumu, mwongozaji anapaswa kutumia vizuri muda alionao kutengeneza filamu nzuri na yenye kuvutia.

UMUHIMU WA DIBAJI KATIKA UANDISHI WA FILAMU.

WATU wengi wamekuwa wakipenda sana kuandika miswada ya filamu, wakifikiria ama kuwa na matumaini kwamba ni rahisi kwao kuweza kuiuza kwa watayarishaji au makampuni mbali mbali yanayotengeneza filamu nchini, na kujipatia kipato lakini wanasahau kwamba kuna vitu vya msingi sana wamekuwa wakisahau kujiuliza ama kuvitafutia ufumbuzi,

Ukweli ni kwamba ni vigumu sana kuandika mswada “script” na kuuuza hasa katika tasnia inayokua kama ya hapa kwetu Tanzania.

Mara nyingi nimekuwa nikipigiwa simu na watu mbali mbali wakiniambia wao ni waandishi wa miswada ya filamu, na wengi wao tayari wameshaandika miswada kadhaa lakini imekuwa vigumu kwao kupata watu wa kuwauzia ama kununua. Wengine wamefika mbali na kuniambia kwamba wako tayari kuniletea ili niweze kuisoma na kuwatafutia wateja.

Kwa nchi za wenzetu kama Marekani, Ulaya na Asia, uandishi wa miswada ya filamu ni biashara na umekuwa ukiwaingizia vipato vikubwa sana waandishi, watu wengi maisha yao yamekuwa yakitegemea taaluma yao ya uandishi wa miswada kwani katika nchi hizo ni biashara kama biashara nyingine lakini hapa kwetu hicho kitu ni tofauti sana, si ajabu ukaambiwa mtu mmoja ndiye aliyeandika mswada, ameuongoza, na pia ameutayarisha ama kuigiza kama mhusika mkuu.

Kwa mfano gharama ya kuandika mswada mmoja wa filamu katika tasnia za wenzetu kama Hollywood au Bollywood ni kati ya dolla za Marekani 3500 – 50,000 (ambazo ni sawa na shilingi milioni 5 mpaka milioni 70 za Tanzania) kwa mswada mmoja wa filamu, na uandishi wa dibaji gharama yake inaanzia dolla 50 mpaka 500 (yaani shilingi 70,000 – 700,000) kwa dibaji moja. Kwa hapa kwetu imekuwa ni vigumu sana kujua ni gharama kiasi gani watayarishaji wamekuwa wanatumia kununua mswada ama dibaji moja.

Ikumbukwe kuwa ni rahisi sana kuuza “wazo“ kuliko kuuza mswada,lakini wazo pekee haliwezi kumpatia pesa mwandishi kwani mara zote wazo linakuwa ni sentensi moja tu, na wala halina maelezo yoyote ya ziada na yanayojitosheleza, ila ni rahisi sana kuuza wazo likiwa pamoja na dibaji.

Pengine unaweza kujiuliza kuwa dibaji “Synopsis” ni kitu gani hasa katika uandishi wa filamu, kwa maelezo yaliyo rahisi unaweza kuielezea dibaji kama ni maelezo mafupi, ya kina ya namna hadithi itakavyokuwa kwenye filamu unayoiandika, inamwelezea mhusika mkuu jinsi alivyoumbwa, muda ama mahali ambapo tukio lilitokea, dibaji pia inaelezea hasa kile kilichomo ndani ya filamu, Pia inaonyesha mwelekeo wa hadithi bila kuelezea mwisho wake.

Jambo la kukumbuka ni kuwa ili dibaji ikamilike ni sharti ielezee au inabeba dhamira kuu ya mswada wa filamu, lakini filamu nyingine zaweza kuwa na dhamira zaidi ya moja na hapo ndipo changamoto inapoibuka, mswada bora wa filamu ni ule ambao unajengwa na dhamira moja huku dhamira zingine zikifanya kazi ya kuimarisha dhamira kuu.

Ukweli ni kwamba hakuna mtayarishaji au mwongozaji atakayekaa ama kukubali kupoteza muda wake kusoma mswada wa filamu yako wenye kurasa 90, au zaidi na kisha aamue kununua au asiununue, bali itakuwa rahisi kwake kusoma dibaji na kujua kila kitu kilichomo kwenye mswada wa filamu yako. Hivyo inashauriwa kuwa wale wote wanaotaka kuwa waandishi wa miswada ya filamu kuzingatia hatua zote za uandishi ikiwa ni pamoja na kuwa na mawazo mapya, ubunifu wa hali ya juu pamoja na kuzingatia mvuto kwa kile wanachokiandika.

Ili mwandishi yeyote wa filamu aweze kuandika vizuri dibaji nzuri na yenye mvuto ni lazima awe mbunifu na wala asiogope kuandika vitu vingi ama maneno mengi kwani hatua zote za uandishi wa dibaji unaenda sambamba na uhariri wa maneno kuanzia mwanzo mpaka mwisho, lakini kabla haujaanza kuandika dibaji yako yakupasa uzingatie mambo haya; kwanza anza kwa kupanga matukio yote ama vitu vyote vinavyotakiwa kwenye mswada wa filamu “ story lines”, unatakiwa awajue wahusika wakuu wa filamu yako, ni kitu gani kiliwatokea? Je ni matukio gani muhimu yaliyomo katika mswada wa filamu unayoiandika?, je wahusika wakuu katka filamu yako wanatumia mbinu gani kupambana na matatizo wanayokabiliana nayo? Je hadithi yako inaishaje? na je ni mabadiliko gani ya kisaikologia ambayo yanatokea mwisho wa filamu yako?

Jambo la kukumbuka ni kwamba unapoandika dibaji ya mswada wako wa filamu zingatia sana kuwa unaiandika kwa kufuata dhamira kuu inataka nini katika hadithi yako, yakupasa uyajibu maswali yaliyoainishwa hapo juu huku ukiandika kitu ambacho ni cha kipekee na chenye mvuto.

Andika sentensi mbili mpaka tatu ambazo unafikiri zimejibu sawia maswali uliyojiuliza hapo juu, mara zote dibaji safi huwa ni fupi, na inaundwa na sentensi mbili au tatu na mara nyingi haizidi paragrafu moja. Ni ukweli usiopingika kuwa ni kazi ngumu kuandika paragrafu moja ambayo itaibeba filamu nzima ya dakika 90, ni dibaji pekee itakayo mshawishi mtayarishaji ama kampuni kununua mswada wako.

Uandishi wa dibaji ni kitu ambacho hakikwepeki hasa kwa mwandishi bora na makini wa miswada ya filamu, daima nitaendelea kuwasisitizia waandishi wote wa miswada ya filamu wajitahidi kadri ya uwezo wao kuzingatia ubunifu, uadilifu na weledi katika kazi wanazoziandika ili waweze kufikia mafanikio ya waandishi wakubwa duniani waingereza wana msemo unaoseama “easy come easy go” wakiwa na maana kuwa mara zote vitu vitavyokuja kirahisi na vitapotea kwa urahisi pia.

Mwandishi anapaswa kukumbuka kuwa uandishi wa filamu ni kazi kama zilivyo kazi zingine, hivyo asiwe ni mtu wa kujirahisisha, wala kuruhusu chembe yoyote ya dharau kwa kile alichokiandika, ni dhambi kumwachia mtu kazi yako ulioiandika bila makubaliano yoyote ya maandishi, daima mwandishi aliye makini na mwelevu baada ya kuandika dibaji ama mswada kitu kinachofuata ni kusajili wazo na mswada wake katika mamlaka za sheria ilikupata haki miliki ya kazi aliyoiandika, nimekuwa nikisikitishwa na malalamiko ya waandishi wengi wakilalama kuibiwa kazi zao, cha ajabu ni kuwa je mamlaka zinzaohusika na usajili ama haki miliki hazipo au hawazioni? au wanapuuzia halafu wananza kulalamika? Waandishi wa filamu kumbukeni kelele za mlango hazimzuii mwenye nyumba kulala, amkeni na mtetee haki zenu.